HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, November 27, 2016

Vodacom Tanzania yapeleka maombi ya kujiunga na Soko la Hisa (DSE)

Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania imetangaza dhamira yake ya kuuza hisa kwa umma itakayofuatiwa na kujiunga kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) ikiwa ni utekelezaji wa sheria ya  Elektroniki na Mawasiliano ya Posta (EPOCA) na sheria ya Fedha ya mwaka 2016 ambayo inaelekeza makampuni ya simu  kumilikisha  asilimia 25 ya hisa zake kwa wananchi kwa kujiunga na Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE).

Akizungumzia  hatua hiyo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Vodacom, Bwana Ian Ferrao alisema “Tunayo furaha kutangaza kuwa tumeanza rasmi mchakato wa kuuza hisa kwa umma kwa mujibu wa matakwa ya sheria na  tumewasilisha maombi na utaratibu mzima utakaotumika kuuza hisa zetu na ratiba yetu nzima kuhusiana mchakato huu kwenye Mamlaka ya Usimamiaji wa  Masoko ya Mitaji  na Dhamana (CMSA) na Soko la Hisa  (DSE).   

Hatua hii ni kubwa na inadhihirisha kuwa Vodacom ipo mstari wa mbele katika kutekeleza agizo la kuuza hisa zake kwa umma  na inadhihirisha jinsi ilivyojipanga  kuendelea kuboresha na kukuza sekta ya mawasiliano nchini Tanzania katika siku za usoni”.

Uuzaji wa hisa kwa umma  na kujiunga na Soko la Hisa kunapitia  hatua mbalimbali za  kupata vibali kutoka taasisi za serikali zenye mamlaka ya kupitia maombi na kutoa  vibali vya utekelezaji wake.Ferrao aliendelea kueleza “Tunaamini uuzaji wa hisa zetu kwa umma utazidi kukuza shughuli za Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE),kunufaisha watanzania kiuchumi na kukuza uchumi wa nchi kwa ujumla.Kampuni yetu haitajulikana kwa jina la mwanzo la Vodacom Tanzania Limited bali imekuwa na jina la Vodacom Tanzania Public Limited Company (Plc) ikiwa ni hatua ya awali ya kujiandaa kuingia sokoni. 

Tunawahakikishia kuwa mchakato wa kuingia kwenye hatua hii umeanza vizuri kwa mafanikio na tunaendelea kuwashirikisha wadau mbalimbali kutoka serikalini kuhakikisha tunatimiza dhamira ya kuanza  kuuza hisa kwa wananchi yenye dira ya kuleta manufaa kwa wote.”

Ferrao alitoa msisitizo kuwa Vodacom inalo jukumu kubwa kuhakikisha hatua hii inaleta manufaa kwa pande zote zinatazohusika kuanzia  wanunuaji wa hisa, kuendelea kuwekeza , kuendelea kuleta mapinduzi ya ubunifu wa kiteknolojia na kuimarisha ubora wa huduma za kampuni kwa wateja wake “Tutaendelea kutoa mchango mkubwa wa ufanikishaji wa sera ya nchi ya miaka 5 ya kukuza sekta ya mawasiliano.Tutaendelea pia kuwaletea taarifa mbalimbali kuhusiana na mchakato wa kuuza hisa kwa umma unavyoendelea”Alisema Ferrao.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Ian Ferrao,(kulia) akimkabidi hati ya maombi ya kujiunga na soko la hisa la Dar es Salaam,(DSE) Mkurugenzi wa Mamlaka ya Masoko na Mitaji na Dhamana (CMSA) Nicodemus Mkama(wapili kushoto) wakati wa hafla fupi iliyofanyike mwishoni mwa wiki katika ofisi za CMSA jijini Dar es Saalaam,Kushoto ni Meneja Uhusiano wa CMSA, Charles Shirima.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Ian Ferrao,(watatu kushoto) akimkabidhi hati ya maombi ya kuijiunga na soko la hisa la Dar es Salaam,(DSE) Mkurugenzi wa Mamlaka ya Masoko na Mitaji na Dhamana(CMSA) Nicodemus Mkama wapili (kushoto) wakati wa hafla fupi iliyofanyike mwishoni mwa wiki katika ofisi za CMSA jijini Dar es Salaam. Wengine kutoka kushoto ni Meneja Uhusiano wa CMSA, Charles Shirima , wanaoshuhudia kutoka Kulia ni Mkurugenzi wa Ushauri wa kutoka huduma za Orbit Securities Company Ltd. Gerase Kamugisha, Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano wa Vodacom Tanzania, Rosalynn Mworia (wapili kulia) na Mkuu wa fedha wa kampuni ya Orbit Securities Company Ltd, Godfrey Gabriel (watatu kutoka kulia).
Mkurugenzi wa Ushauri wa kutoka huduma za Orbit Securities Company Ltd. Gerase Kamugisha(kushoto)Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Ian Ferrao, Mkurugenzi Mtendaji wa DSE,Moremi Marwa, Mkuu wa masuala ya kifedha wa Orbit Securities Company Ltd, Godfrey Gabriel, Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano wa Vodacom Tanzania, Rosalynn Mworia,wakionyesha hati za maombi ya kuijiunga na soko la hisa la Dar es Salaam,(DSE) mwishoni mwa wiki.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad