HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, November 11, 2016

BOT YASITISHA KUWEKA DHAHABU KAMA HAZINA YA RASILIMALI ZA KIGENI

Benki Kuu ya Tanzania (BOT) imesitisha kuweka dhahabu kama hazina ya rasilimali za kigeni kwa sababu ya kuyumba kwa bei ya madini hayo katika soko la dunia na kusababisha uwezekano wa kupunguza thamani ya hazina ya rasilimali ya nchi.

Kauli hiyo imetolewa jana mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt Ashatu Kijaji alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Igunga Mhe. Dalaly Kafumu aliyehitaji kufahamu sababu za Serikali kukataa kutunza dhahabu safi katika Benki Kuu wakati Tanzania ni nchi mojawapo inayozalisha dhahabu safi.

Mhe. Kijaji alisema kuwa jukumu la msingi la Benki Kuu ni kuandaa na kutekeleza Sera ya Fedha inayolenga kuwa na utulivu wa bei kwa ajili ya ukuaji endelevu wa uchumi wa Taifa hivyo ili kufanikisha azma hiyo Benki Kuu inadhibiti ongezeko la ujazi wa fedha kwa kutumia nyenzo mbalimbali zikiwemo za kuuza dhamana na hati fungani za Serikali pamoja na kushiriki katika soko la jumla la fedha za kigeni kati ya mabenki.

“Katika kutekeleza jukumu lake la msingi, Benki Kuu hutunza hazina ya rasilimali za kigeni zinazotosha kuagiza bidhaa nje kwa kipindi kisichopungua miezi minne lakini kwa muda mrefu sasa Benki Kuu ya Tanzania haiweki dhahabu kama sehemu ya rasilimali hizo kutokana na kuyumba kwa bei ya dhahabu katika soko la dunia”, alisema Mhe. Kijaji.

Naibu Waziri huyo alitoa mfano wa kushuka kwa bei ya dhahabu katika soko la Dunia ambapo dhahabu ilishuka kutoka dola 1,745 za kimarekani katika mwezi Septemba 2012 hadi dola za kimarekani 1,068 kufikia mwezi Desemba 2015.

Mhe. Kijaji alifafanua kuwa hazina ya rasilimali za kigeni zinaweza kuwa dhahabu – fedha (monetary gold) au fedha za kigeni ambapo uamuzi kuhusu hazina itunzwe vipi unazingatia vigezo mbalimbali vikiwemo vile vya kudumisha thamani, wepesi wa kubadilisha pamoja na faida inayopatikana kwa kuwekeza hazina hiyo.

Aidha, Mhe. Kijazi alisema kuwa ununuzi na uuzaji wa madini ya dhahabu unahitaji ujuzi maalum ambapo kwa kuzingatia jukumu la msingi la Benki Kuu inaonyesha dhahiri kuwa Benki hiyo haijajijengea uwezo katika eneo la biashara ya madini hayo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad