Rais Dkt John Pombe Magufuli
Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, kesho tarehe 31 Oktoba, 2016
ataanza ziara ya Kiserikali ya siku mbili nchini Kenya kwa mwaliko wa Rais wa
Jamhuri ya Kenya Mhe. Uhuru Kenyatta.
Rais Magufuli
anatarajiwa kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta
Jijini Nairobi majira ya saa nne asubuhi na baadaye kupokelewa rasmi na
mwenyeji wake Rais Kenyatta katika Ikulu ya Nairobi ambako viongozi hao
watafanya mazungumzo rasmi.
Pamoja na kufanya
mazungumzo rasmi na mwenyeji wake, Rais Magufuli atakwenda kutoa heshima katika
Kaburi la Rais wa Kwanza wa Kenya Hayati Mzee Jomo Kenyatta na pia anatarajiwa
kuhudhuria dhifa ya kitaifa aliyoandaliwa na mwenyeji wake Rais Uhuru Kenyatta
Ikulu Jijini Nairobi
Katika ziara hii
Rais Magufuli anatarajiwa kutembelea kiwanda cha maziwa cha Eldoville kilichopo Karen Jijini Nairobi, na
pia anatarajiwa kuzindua barabara mchepuko ya Southern By-pass iliyopo Jijini Nairobi.
Barabara hiyo
mchepuko ya Southern By-pass ni moja
kati ya miradi mikubwa ya barabara nchini Kenya, inaunganisha maeneo mbalimbali
ya Jiji la Nairobi kwa barabara za juu na chini na imejengwa kwa lengo la
kupunguza msongamano wa magari katika Jiji hilo.
Rais Magufuli
anatarajiwa kumaliza ziara yake tarehe 01 Novemba, 2016 na kurejea Jijini Dar
es Salaam.
Gerson
Msigwa
Mkurugenzi
wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Nairobi
30 Oktoba,
2016.
No comments:
Post a Comment