HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 29, 2016

Paul Mashauri awataka vijana kufanya kazi kwa bidii ili kuondokana na umaskini

Katika kuhakikisha kuwa Tanzania inakuwa nchi yenye maendeleo na iliyo na watu ambao wamefanikiwa kimaisha, vijana nchini wametakiwa kufanya kazi kwa bidii ili kujikomboa na janga la umaskini lakini pia kulisaidia taifa kupata maendeleo.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya HiTech International, Paul Mashauri wakati akizungumza na vijana ambao wanajifunza ujasiriamali na kuwambia ni vyema wakaongeza bidii katika ndoto wanazotamani kuzifikia ambazo pia zitawasaidia kuondokana na umaskini ambao umekithiri nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya HiTech International, Paul Mashauri akizungumza na vijana kuhusu ujasiriamali.

Alisema ili mtu kufanikiwa kimaisha haitaji zaidi elimu ya darasani bali ni muhusika mwenyewe kujiongeza kwa kufanya kazi kwa bidii katika jambo ambalo anatamani kulifikia na akiwatolea mfano yeye mwenyewe kuwa tangu amalize masomo yake katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam hajawahi kurudi chuoni kuchukua cheti chake lakini amefanikiwa kimaisha.

"Mimi simchukii mtu ila nauchukia umaskini alionao, ukiwa na juhudi katika biashara na kujituma hata Rais Magufuli hatakufikia mshahara watu wanaweza kusema unafanya biashara ya kawaida lakini inakulipa sana, ni wewe tu na juhudi zako unazofanya ili ufanikiwe,

"Maisha hayana formula kuwa kufanikiwa ni lazima uwe na masters ndiyo upate mafanikio, masters ya maisha ni kuwa mtaani maisha yakupige alafu uinuke upambane na uyashinde hapo ndiyo umeyashinda maisha, ukitaka kufanikiwa lazima ufanye kazi kwa bidii hata mimi natumia muda wangu mwingi kujifunza ili nizidi kufanikiwa," alisema Mashauri.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya HiTech International, Paul Mashauri akiwaeleza vijana jinsi wanavyoweza kufanikiwa kimaisha kwa kufanya biashara.

Aidha Mashauri aliwataka vijana hao kutumia fursa ambayo inatolewa na kampuni yake ya kuuza vifaa vya viwandani ya HiTech International kwa kuwapatia mkopo wa mashine watu ambao wanatamani kufanya biashara za aina mbalimbali ili waweze kufanikiwa kama matajiri wengine wakubwa nchini wamevyofanikiwa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya HiTech International, Paul Mashauri akiwaonyesha moja ya mashine ambazo Kampuni ya HiTech International inaziuza.

Nae mwendesha mafunzo kwa vijana hao kutoka Shirika la Kazi Duniani (ILO), Benny Mwambela alisema mafunzo hayo yameanzishwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni na Shirika la Kazi Duniani (ILO) ili kuwasaidia vijana kupata mbinu za jinsi gani wanaweza kufanikiwa kibiashara na baada ya mafunzo hayo, wahitimu watakwenda kutoa elimu kwa vijana wengine.

"Tunafundisha walimu ambao watakwenda kufundisha watu wengine kuhusu ujasiriamali, kuna watu wasiopungua 10,000 wamejiandikisha kujifunza ujasiriamali kwahiyo tunawafundisha watu hawa ili wakawafunze na wengine ili na wao wajue jinsi gani wanaweza kufanya biashara,

"Wanafundishwa jinsi ya kubuni wazo la biashara, kuna wengine wana mawazo ya biashara watafundishwa jinsi ya kuanzisha biashara, na kuna wengine wanafanya biashara wanafundishwa jinsi ya kutanua biashara na watafundishwa kuhusu kuanzisha vikundi na jinsi gani ya kutumia fedha," alisema Mwambela.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya HiTech International, Paul Mashauri akiwaeleza vijana jinsi wanavyoweza kuepuka umaskini kwa kufanya kazi kwa bidii.
Baadhi ya vijana walioshiriki semina hiyo.


Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya HiTech International, Paul Mashauri akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, waendeshaji wa mafunzo na washiriki wa mafunzo. (Picha zote na Rabi Hume)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad