Na Grace Michael
MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu ameupongeza Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kwa kazi nzuri na
kubwa ya upimaji wa afya za wananchi iliyofanyika katika maonesho ya Kitaifa ya Nane Nane mkoani
Lindi.
Pongezi hizo alizitoa wakati alipotembelea banda hilo katika kilele cha maonesho hayo ambapo
alisema kuwa kazi inayofanywa na Mfuko inawasaidia wananchi kutambua afya zao lakini pia elimu
ya kuepukana na maradhi yasiyoambukizwa.
“NHIF nawapongeza sana kwa kazi kubwa mliyoifanya mahali hapa, nimepata taarifa zenu kwamba
mnapima afya za wananchi bure...hongereni sana na fursa hii iwafikie na wengine” alisema Makamu
wa Rais.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Bernard Konga akitoa
maelezo ya huduma zilizotolewa na Mfuko katika maonesho ya Nane Nane mkoani Lindi kwa
Makamu wa Rais, Samia Suluhu wakati alipotembelea banda hilo. Kati kati ni Mwenyekiti wa
Bodi ya NHIF, Mama Anne Makinda.
Katika maonesho hayo, Mfuko ulitoa huduma mbali zikiwemo za elimu ya namna ya kunufaika na
huduma za Mfuko, usajili wa wanachama wa Mfuko wa Afya ya Jamii, upimaji wa afya kwa wananchi
ikiwemo saratani ya matiti, hali lishe, sukari na shinikizo la damu pamoja na elimu ya kuepukana na
magonjwa hayo.
Kwa upande wa Mwenyekiti wa Bodi ya NHIF, Mama Anne Makinda alitoa mwito kwa Watanzania
kuhakikisha wanatumia fursa zinazotolewa na Mfuko ikiwemo kujiunga na huduma za Mfuko ili
wawe na uhakika wa kupata huduma za matibabu wakati wowote.
Meneja wa Mkoa wa Lindi Fortunata Raymond akitoa maelezo ya huduma kwa Mwenyekiti
wa Bodi ya NHIF, Mama Anne Makinda alipotembelea kuona huduma zinazotolewa.
Alisema kuwa Mfuko umejipanga kuhakikisha unahudumia idadi kubwa ya Watanzania hivyo ni
vyema wakachangamkia huduma zilizopo kwa kuwa zinagusa makundi mbalimbali yakiwemo ya
Watoto, wanafunzi, watu binafsi, wajasiliamali na makundi mengine.
“Nawahamasisha tu Watanzania kujiunga na huduma za Mfuko huu kwani zimezingatia mahitaji ya
kila Mtanzania na huu ndio mpango wa Serikali wa kuhakikisha kila mwananchi anakuwa kwenye
Mfumo wa Bima ya Afya,” alisema Mama Makinda.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Mfuko Bw. Bernard Konga aliwahakikishia Watanzania kuwa, Mfuko uko
imara na umejipanga kutoa huduma bora ambazo zitakidhi mahitaji yao.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Simbachawene
akizungumza na Meneja wa NHIF Lindi baada ya kuona huduma zinazotolewa na Mfuko huo.
Alisema kuwa Mfuko unaendelea kufanya maboresho mbalimbali katika huduma zake kwa
kuzingatia makundi mbalimbali ya wananchi ili kuwezesha mpango wa Serikali wa afya bora kwa
wote.
“Tunaendelea na kasi ya utoaji wa elimu ya huduma zetu kwa wananchi na kwa sasa huduma zetu
zipo mpaka ngazi ya chini kabisa kwa kuwa tuna ofisi za Mfuko kila mkoa zinazofanya kazi ya
kuwafikia wananchi mpaka ngazi ya kaya,” alisema Bw. Konga.
Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Dr, Charles Tizeba akitoa maelekezo kwa Kaimu
Mkurugenzi wa NHIF, Bernard Konga katika banda la Mfuko.
Wananchi wakiwa katika banda la Mfuko kwa ajili ya kupata huduma za elimu na upimaji wa
afya zao.
Maofisa wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya wakiwajibika kuwahudumia wananchi.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Simbachawene
akipima uzito katika banda la NHIF ambalo lilitoa huduma mbalimbali.
Meneja wa NHIF Mkoa wa Lindi akitoa elimu kwa wananchi.
Mwenyekiti wa Bodi ya NHIF Mama Anne Makinda akiwa katika picha ya pamoja na
watumishi wa Mfuko baada ya kumalizika kwa maonesho ya Kitaifa Nane Nane.
No comments:
Post a Comment