HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, June 27, 2016

BUNGE LIMEPITISHA MUSWADA WA MAREKEBISHO YA SHERIA YA ELIMU.


 Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Amina Mollel  akiuliza swali Bungeni leo wakati wa kipindi cha maswali na majibu kuhusu hatua zinazochukuliwa na Serikali kuwawezesha wanafunzi wenye Ulemavu sawa na wale wasio na ulemavu hasa kwa kuangalia miundombinu iliyopo ili iwe rafiki kwa kundi hilo na kuleta usawa katika kupata elimu.
 Naibu Waziri Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia Injinia Stella Manyanya akitoa ufafanuzi leo Bungeni Mjini Dodoma kuhusu hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha kuwa wanafunzi wenye ulemavu wanapata elimu sawa na wale wasio na ulemavu kwa kuweka miundo mbinu rafiki katika shule na vyuo vyote nchini.
 Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. George Masaju akijibu hoja za Wabunge mapema leo Bungeni  Mjini Dodoma wakati akihitimisha hoja kuhusu muswaada wa sheria ya marekebisho ya sheria mbalimbali  wa mwaka 2016.
 Naibu Spika,Dkt. Tulia Ackson akiteta jambo na Mbunge Viti Maalum Mhe. Kiteto Zawadi Koshuma katika viwanja vya Bunge, mjini Dodoma.
(Picha zote na Frank Mvungi – MAELEZO - Dodoma)

Na: Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma. 
Bunge la Jamhuri wa Muungano wa Tanzania leo, Mjini Dodoma limepitisha muswada wa marekebisho ya sheria ya Elimu kifungu kinachoeleza kuwa mtu anayempatia ujauzito mwanafunzi wa shule ya msingi au sekondari kuwa adhabu yake ni faini isiyozidi shilingi laki tano au kifungo kisichozidi  miaka mitatu.

“Muswada unapendekeza kuwa kifungu hicho kifutwe na badala yake kitungwe kifungu kipya cha 60A ili kuweka masharti yanayojitosheleza kuhusu zuio la kuoa au kumpatia ujauzito mwanafunzi wa shule ya msingi au sekondari, kinapendekeza adhabu yake iwe kifungo cha miaka 30 gerezani,” alifafanua Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. George Masaju.

Vile vile mtu atakayebainika kusaidia, kushawishi au kuacha mwanafunzi wa shule ya msingi au sekondari kuolewa au kuoa anatenda kosa la jinai ambalo adhabu yake ni faini isiyopungua shilingi milioni tano au kifungo cha miaka mitano gerezani au vyote kwa pamoja.

Mhe. Masaju aliendelea kwa kufafanua kuwa, sheria hiyo imependekeza kuwa pale ambapo kosa hilo litafanywa na mtoto basi adhabu yake itakuwa kwa mujibu wa masharti ya sheria ya mtoto. Hii ni kwa sababu sheria ya mtoto inakataza mtoto anayetiwa hatiani kufungwa gerezani.

Aidha marekebisho hayo katika sheria ya Elimu yanalenga kumjengea mwanafunzi wa shule ya msingi au sekondari mazingira mazuri ya kumaliza ipasavyo elimu yake kwa ngazi hiyo.Hivyo basi kila Mkuu wa shule au Mwalimu Mkuu atawasilisha kwa Kamishna wa Elimu taarifa ya robo mwaka kuhusu matukio ya ndoa na mimba kwa wanafunzi katika shule yake na hatua zilizochukuliwa.

Sheria ya Elimu inamruhusu mwanafunzi aliyepewa ujauzito kuendelea na masomo mara tu anapojifungua. Sheria hiyo inasubiri kuwekwa saini na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli ili ianze kutumika.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad