HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, October 13, 2015

Maandalizi ya Rotary Dar Marathon 2015 yakamilika

Naibu mkurugenzi mkuu wa Benki M Bi. Jacqueline Woiso akiongea na waandishi wa habari leo hii katika ukumbi wa Hyatt Regency juu ya maandalizi ya Rotary Dar Marathon 2015 ambayo huandaliwa na Rotary klabu za Dar es salaam kwa kushirikiana na Benki M. Mbio na matembezi ya Dar Rotary Marathon kwa mwaka huu zitafanyika katika viwanja vya Green, Oysterbay tarehe 14 October 2015. Kutoka kushoto ni Mwenyekiti wa bodi ya Rotary Bi. Sharmila Bhatt, Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi Bi. Agnes Batengas, Makamu wa Raisi wa Rotary klabu Oysterbay Bi. Anne Saels na Rais wa Rotary Klabu Dar North Bw. Masato Wassira.
baadhi ya washiriki wa Rotary Dar Marathon kutoka Malawi na Kenya wakifuatilia mkutano huo, Marathon ya mwaka huu itajumuisha wakimbiaji kutoka nchi za Kenya, Rwanda, Malawi, South Africa na Ethiopia.

Mbio na matembezi ya hisani za Dar rotary marathon yanatarajiwa kufanyika siku ya jumatano tarehe 14.10.2015 hapa jijini Dar es salaam ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa rais mstaafu mheshimiwa Ally Hassan Mwinyi. 

Mbio na matembezi hayo yameandaliwa na klabu sita za Rotary za hapa Dar es salaam kwa kushirikiana na Benki M na kauli mbiu ya mwaka huu ni “kuponya maisha, badilisha jamii” ambapo fedha zitakazochangishwa ziltaelekezwa katika ujenzi wa kituo cha afya hapa Dar es salaam. 

 Akiongea na waandishi wa habari jijini Dar es salaam jana kuhusu maandalizi, mwenyekiti wa kamati ya maandalizi Bi. Agnes Batengas alisema kuwa kamati yake imejiandaa vilivyo na maandalizi yote yamekamilika, ikiwemo kupokea wakimbiaji kutoka nje ya nchi na washiriki wengine.

Aliongeza kuwa mbio hizo huwa zina lengo la kuchangisha fedha za kusaidia kupunguza changamoto zinaoikabili jamii yetu, kama ilivyo mwaka huu ambapo tutajenga kituo cha afya.

Bi. Batengas alisema kuwa wanatarajiwa kuwa na washiriki wapatao zaidi ya 13,000 ambapo kutakuwa na matembezi ya kilomita 5 kwa ajili ya familia, kilomita 9 na mbio za kilomita 21.1 nusu marathon, halikadhalika kutakuwa na waendesha baiskeli. 

Matembezi na mbio hizo zitaanzia na kuishia katika viwanja vya Green, Oysterbay ambapo wakimbiaji na waendesha baiskeli wataanza saa 12 asubuhi na watemebeaji wataanza saa 1 asubuhi. Barabara maarufu za jijini zitatumika ikiwemo Toure Drive, Chole, Haile sellasie, Alli Hassan Mwinyi, Obama, Kivukoni, Ohio na Kenyatta.

Kuhusiana na usalama katika tukio hilo ambalo litahusisha maelfu ya watu, Bi. Batengas alisema “tumekuwa tukifanya kazi kwa ukaribu sana na jeshi la polisi, hivyo jeshi la polisi limeshajipanga vilivyo kwa ajili ya tukio hilo ili kuhakikisha kila kitu kinaisha kwa usalama”, alisema.

Naye naibu katibu mkuu wa chama cha riadha Tanzania Bi. Ombeni Zavala alisema kuwa mamlaka zote zimehusishwa katika kuandaa tukio hili, “tumekuwa tukifanya kazi kwa kushirikiana na kamati ya maandalizi ya Dar Rotary marathon kwa muda mrefu na tumekuwa tukihakikisha kila marathon wanayoandaa inafanyika katika viwango vya kimataifa.

Mwenyekiti wa bodi ya Rpotary, Bi. Sharmilla Bhatt aliongeza kuwa Marathon ya mwaka huu itakuwa na wakimbiaji kutoka kila pembe ya Africa. “Muitikio kutoka nchi za jirani ni mkubwa, wakimbiaji kutoka Kenya, Rwanda, Malawi, Afrika Kusini na Ethiopia wamethibitisha kushiriki. Na tutaongeza nchi nyingi zaidi mwaka ujao wa 2016 kwa kuwa umaarufu wa Dar Rotary marathon unazidi kuongezeka siku hadi siku na nchi nyingi ziko tayari kuleta wakimbiaji wao maarufu kabisa kuja kushiriki. Jumla ya washiriki 13,000 wanatarajiwa kushiriki Marathon ya mwaka huu”.

Akichangia juu ya ushiriki wa Benki M katika mbio na matembezi haya, Naibu mkurugenzi mkuu wa benki hiyo Bi. Jacqueline Woiso alisema kuwa wamekuwa wakishiriki katika shughuli mbalimbali maendeleo ya jamii, hivyo wamekuwa wakishirikiana na Rotary katika Rotary Dar marathon toka ilipoanzishwa mwaka 2009.

Aliongeza kuwa “ni sera yetu kushirikiana na taasisi mbalimbali zinazoheshimika katika kuleta mageuzi kwa wahitaji hapa nchini, tunaamini kabisa kuwa kwa pamoja tukishirikiana tutafanikisha ujenzi wa kituo hiki cha afya hapa Dar es salaam. Hii ina maana kubwa sana kwetu kuiona sekta ya afya katika jamii yetu inapewa kipaumbele”.

Mbali na Benki M ambaye ndiye mdhamini mkuu, wadhamini wengine ni SBC (Pepsi), Spicenet, Soft tech, Toyota, Ultimate Security, Security Printers, Copy Cat, ALAF, Azam Tv, BG Tanzania na Grand malt.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad