HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, July 24, 2014

KUWENI MAKINI NA TAASISI ZA FEDHA FEKI - SERIKALI

Na Rose Masaka-MAELEZO-Dar es Salaam.

Serikali imewataka  wananchi       kujihadhari na wizi ambao hufanywa na Taasisi za Fedha hewa ambazo zimekuwa zikidai kutoa mikopo kwa njia ya simu.

Tahadhari hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi wa Idara ya Habari(MAELEZO) Assah Mwambene wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam.

Amesema kuwa Taasisi hizo zimekuwa zikitumia  mitandao ya simu za mkononi kutapeli wananchi kwa kuwaraghai kuwa watawapatia mikopo.

Mwambene ameongeza kuwa Taasisi hizo zimekuwa zikitumia majina ya viongozi wakubwa mbalimbali wa vyama na Serikali kuwatapeli wananchi kwa kuwachukulia fedha zao.

Amesema kuwa baadhi ya taasisi hizo zinatumia namba za uongo za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwaibia wananchi.

Mkurugenzi huyo amezitaja baadhi ya Taasisi hizo kuwa ni pamoja na Social credit Loans ambayo inadai  imesajiliwa na TRA kwa namba Reg.No.33/SCC/REG/7894 na namba ya utambulisho wa mlipa kodi ni TIN:203-344-6789.

Taasisi nyingine ni Saving Foundation na Quicken Loan ambazo zote hizo zimekuwa zinawatapeli wananchi.

Amesema kuwa baada ya kuwasiliana Mamlaka ya Mapato Tanzania, imebainika kuwa hakuna taarifa yoyote kuhusu Taasisi hizo. 

Mwambene amesema kuwa Serikali inaendelea kufanyia uchunguzi ili wahusika waweze kukamatwa na kuchukuliwa hatua.

Aidha , Mkurugenzi huyo amewakumbusha wananchi kutokubali maombi ya fedha, fadhila au maelekezo yanayodaiwa kutolewa na uongozi wa juu bila kupata uthibitisho kutoka mamlaka husika.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad