Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Vijana,
Utamaduni na Michezo, Bw. Sethi Kamuhanda ametangaza rasmi nembo ambayo
itatumika katika madhimisho ya miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara.
Bw. Kamuhanda ametangaza nembo hiyo
leo jijini Dar es Salaam na kusema kuwa wakati nchi yetu ikisherehekea
miaka 50 ya Uhuru Serikali kupitia kamati ya kitaifa ya maadhimisho
imeandaa nembo rasmi ya maadhimisho hayo.
Pamoja na ubunifu mwingine uliopo katika
nembo hiyo, kuna ujumbe pia unaosomeka kuwa TUMETHUBUTU, TUMEWEZA, TUNAZIDI
KUSONGA MBELE.
Akieleza maana ya maneno hayo amesema
kuwa kuthubutu ni kufanya jambo kwa ujasili na kusema kuwa, kwa ujasili
mkubwa nchi Yetu imethubutu kudai uhuru, imethubutu kujenga umoja miongoni
mwa wananchi, imethubutu kuwa na muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar
na tumethubutu kujiletea maendeleo katika sekta mbalimbali za kijamii,
kiuchumi na kisiasa.
Amesema kuwa katika masuala yote tuliyothubu
tumeweza kuyafanikisha na ni dhahiri kuwa taifa limeendelea katika sekta
mbalimbali na tunazidi kusonga mbele ili kujiletea maendeleo zaidi.
Aidha, amevitaka vyombo vya habari
nchini kuhakikisha kuwa vinaitangaza nembo hii ili wananchi waweze kuielewa
vizuri. Pia ameyataka makampuni ya watu binafsi kuhakikisha
kuwa wanaitumia nembo hii katika maeneo yao na katika machapisho yao
mbalimbali.
Wakati huhuo, amezungumzia suala la
kufungwa kwa Uwanja wa Taifa baada ya mchezo wa Ngao ya Hisani uliochezwa
kati ya Simba na Yanga tarehe 17 Agosti, 2001 kuwa baada mechi ile kulitokea
uharibifu wa vifaa ambavyo vilihitaji matengenezo kabla ya matumizi
ya Uwanja.
Bw. Kamuhanda ameeleza kuwa wataalam
wa viwanja waliishauri Wizara kuwa uwanja ule unatakiwa kutumika si
zaidi ya mara mbili kwa wiki kwa kuwa majani yale ni ya asili na yanahitaji
kutunzwa.
Amesema kuwa Wizara imeshawasiliana
na TFF kwa kuwa ndio wenye jukumu la kupokea maombi kutoka kwa vilabu
kwa ajili ya kutumia uwanja ule, ili wanapoletewa maombi hayo wazingatie
masharti ya matumizi ya Uwanja huo.
Ameeleza kuwa mechi za Kimataifa pamoja
na zile zinazohusisha vilabu na Timu za kimataifa zitaruhusiwa kutumia
uwanja huo lakini kwa kuzingatia ushauri uliotolewa na wataalamu wa
viwanja kuhusu matumizi ya uwanja huo.
No comments:
Post a Comment